October 6, 2024

Tanzania yapokea msaada wa vifaa tiba kupambana na Corona

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsi, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema Tanzania imepokea msaada wa vifaa tiba vya kupambana na maambukizi ya virusi vya corona ambavyo vimetolewa na Bilionea wa China, Jack Ma.

  • Ni vile vilivyotolewa na Bilionea wa China Jack Ma.
  • Vitasaidia kupima na kuwakinga wagonjwa wa Corona. 

Dar es Salaam. Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsi, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema Tanzania imepokea msaada wa vifaa tiba vya kupambana na maambukizi ya virusi vya corona ambavyo vimetolewa na Bilionea wa China, Jack Ma.

Ummy amesema shehena ya vifaa hivyo iliwasili jana usiku kwa ndege ya Shirika la ndege la Ethiopia (Ethiopia Airlines) na kupokelewa na maafisa wa afya. 

โ€œJana usiku Tanzania imepokea msaada wa vifaa tiba ambavyo vitasaidia kupambana dhidi ya virusi vya Corona,โ€ ameandika Ummy katika ukurasa wake wa Twitter leo (Machi 25, 2020).

Kutokana na msaada huo amemshukuru Ma na Waziri Mkuu wa Ethiopia, Abiy Ahmed ambaye amekuwa mstari mbele kuhamasisha matajiri na wafanyabiashara duniani kuzisaidia nchi za Afrika kupata vifaa vitakavyosaidia kutokomeza ugonjwa huo unaosambaa kwa kasi duniani.

Baadhi ya nchi za Afrika zilizopata msaada huo ni pamoja na Ghana, Congo, Congo DRC, Somalia, Ethiopia.

Kwa mujibu wa Ahmed shehena ya pili ya vifaa tiba vilivyotolewa na Ma iko njiani na itaingia Ethiopia muda wowote kuanzia sasa kabla ya kusambazwa katika nchi za Afrika ambazo zimeathirika na ugonjwa huo.


Zinazohusiana


Vifaa tiba vilivyotolewa ni pamoja na barakoa na mashine za kupima wagonjwa wa ugonjwa huo ambao hauna dawa wala chanjo. 

Machi 22, 2020 Ahmed alitangaza kuwa Ma na kampuni yake @AlibabaGroup wametuma shehena ya kwanza ya vifaa tiba vikiwemo barakoa milioni 6, vifaa milioni 1.1 vya kupima corona na mavazi ya kujikinga 60,000 ya wahudumu wa afya ambavyo vitasambazwa katika nchi za Afrika.

Kwa mujibu wa Kituo cha Afrika cha kuzuia na kudhibiti magonjwa (CDC Afrika) mpaka leo (Machi 25, 2020) nchi 43 za bara hilo zimethibitisha kuwa na wagonjwa wa Corona ambapo watu 64 wamefariki kutokana na ugonjwa huo.

Katika hatua nyingine, Waziri Ummy anatarajia kuongea na waandishi wa habari leo mchana kutoa ufafanuzi wa mambo mbalimbali kuhusu ugonjwa huo.