October 6, 2024

Ajikuta amekuwa fundi bomba badala ya sonara baada ya kuchanganya lugha

Ni mkimbizi wa Syria, Safaa Sukarria aliyeko ukimbizi nchini Jordan ambaye amejikuta akiingia katika kazi hiyo baada ya kukosea kuelewa neno la kiarabu la ‘sabaka’ ambalo kwao Syria linahusika na uyeyushaji vyuma na vito, huku nchini Jordan likimaanisha uf

Safaa Sukarria (katikati) akiwaelekeza wanawake wenzake namna nzuri ya kutumia vifaa vya kutengeneza mabomba ya vyoo. Picha|UNHCR.


  • Ni mkimbizi wa Syria, Safaa Sukarria aliyeko ukimbizi nchini Jordan ambaye amejikuta akipata ujuzi wa kutengeneza mabomba baada ya kushindwa kuwasiliana vizuri na wenyeji wake. 
  • Alijikuta akiingia katika kazi hiyo baada ya kukosea kuelewa neno la kiarabu la ‘sabaka’ ambalo kwao Syria linahusika na uyeyushaji vyuma na vito, huku nchini Jordan likimaanisha ufundi bomba.

Lugha ni nyenzo muhimu ya mawasiliano inayowaunganisha watu wa rika tofauti katika shughuli mbalimbali za uzalishaji. Kama watu watashindwa kuelewana katika lugha wanayoongea ni rahisi kwa mambo mengi kukwama hasa yale yanayogusa maendeleo ya eneo fulani. 

Lakini wakati mwingine, kutoelewana katika kile mnachozungumza inaweza ikawa fursa muhimu kwa watu kutengeneza mstakabali mzuri wa maisha yao.

Hivi ndivyo ilivyomtokea mkimbizi wa Syria, Safaa Sukarria aliyeko ukimbizi nchini Jordan ambaye amejikuta akipata ujuzi wa kutengeneza mabomba baada ya kushindwa kuwasiliana vizuri na wenyeji wake. 

Video iliyoandaliwa na shirika la kuhudumia wakimbizi duniani (UNHCR), inamuonesha mkimbizi Sukarria akiwa nchini Jordan,  ambaye amejikuta akiwa fundi bomba na hata kufundisha wenzake kazi hiyo huko ukimbizini licha ya kwamba kazi yake alikotoka alikuwa ni sonara.

Nchini Syria alikuwa Sonara na alipokimbilia Jordan akataka kujiendeleza kwa fani yake lakini ikawa tofauti analivyodhani. 

Kwa mujibu wa UNHCR, alijikuta akiingia katika kazi ya ufundi bomba ukimbizini Jordan baada ya kukosea kuelewa neno la kiarabu la ‘sabaka’ ambalo kwao Syria linahusika na uyeyushaji vyuma na vito, huku nchini Jordan likimaanisha ufundi bomba.

“Nilijiandikisha kwenye semina ya utengenezaji wa vito. Lakini kumbe nikakuta ni mafunzo ya ufundi bomba,” anaeleza Sukarria katika video hiyo.


Zinazohusiana:


Sukarria anaonekana akiwaelekeza wanawake wenzake kukarabati mabomba ya maji na ya vyoo.

Kwa kuanzia, alikuwa anawatengenezea mabomba ndugu na jamaa. Lakini baadaye shughuli ikakua akawafundisha wanawake 25; ambao wamekuwa sehemu ya  kikosi chake cha mafundi wakikarabati mabomba, matanki ya maji na vyoo. 

“Siyo kazi ya mwanaume au mwanamke. Ni suala la ujuzi. Baadhi ya wanaume wananiambia kwa hivyo wewe ni mwanamke mwenye misuli yenye nguvu, unafikiri wewe ni mwanaume? Ninapata maoni mengi kama hayo lakini ninayapuuza,” amesema Sukarria.

Kwa sasa, Sukarria anamiliki biashara nchi nzima ya Jordan na pia kituo pekee katika ukanda huo cha kufundisha wanawake kazi ya ufundi bomba.

Sukarria ni miongoni mwa wanawake wengi waliopo Tanzania ambao wanatumia ujuzi na uwezo walionao kubadilisha maisha ya watu wengine licha ya vikwazo vingine hasa mfumo dume vinavyowakwamisha.