October 6, 2024

Rasmi Kamishna Diwani Athumani bosi Takukuru

Kabla ya uteuzi huo mpya alikuwa Katibu Tawala Mkoa wa Kagera.

  • Kabla ya uteuzi huo mpya alikuwa Katibu Tawala Mkoa wa Kagera.
  • Pia amewahi kuwa Kamanda wa Polisi katika mikoa ya Shinyanga na Mbeya.
  • Anachukua nafasi ya Kamishna Valentino Mlowola aliyeteuliwa kuwa Balozi.

Kamishna wa Polisi Diwani Athumani rasmi ni Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru). Picha| Mwananchi.

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amemteua Kamishna wa Polisi Diwani Athumani kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na utezi wake unaanza rasmi leo Septemba 6, 2018. 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, Kamishna Athumani anachukua nafasi ya Kamishna wa Polisi, Valentino Mlowola ambaye ameteuliwa kuwa Balozi. 

Kamishna Athumani aliyewahi kuwa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), kabla ya uteuzi huo mpya alikuwa Katibu Tawala Mkoa wa Kagera. Pia aliwahi kuwa Kamanda wa Polisi katika mikoa ya Shinyanga na Mbeya.

Kwa upande wake, Kamishna Mlowola chati yake imezidi kupanda ikizingatiwa kuwa aliteuliwa kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU Disemba 2015 baada ya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa taasisi hiyo wa wakati huo, Dk Edward Hoseah kutokana na kutoridhishwa na namna taasisi hiyo ilivyokuwa ikitekeleza wajibu wake katika kukabiliana na rushwa hususani kwenye upotevu wa mapato ya serikali katika bandari ya Dar es salaam.