July 8, 2024

Fahamu Mapori 10 makubwa ya akiba Tanzania

Mapori hayo ya kiba kwa pamoja yana ukubwa wa eneo la kilomita za mraba zipatazo 96,146.

  • Mapori hayo ya kiba kwa pamoja yana ukubwa wa eneo la kilomita za mraba zipatazo 96,146.
  • Ukubwa wa mapori hayo 10 ni zaidi ya mikoa sita ya Tanzania bara.

Dar es Salaam. Ni nadra sana kwa Tanzania kukuta maelezo kuhusu vitu vya kihistoria kwenye mitandao ya kijamii. Licha ya baadhi ya taarifa kuwepo mtandaoni, ni mara chache kupata uchambuzi wa kina utakaokupa ufahamu. Mfano, je wafahamu mapori makubwa 10 ya akiba Tanzania ambayo ni moja ya vivutio vya utalii? 

Kama hata  bado unakabiliana na changamoto hiyo ya kusaka habari ya mapori 10  ya akiba,  usiwaze. Nukta (www.nukta.co.tz) inakuletea orodha ya  mapori 10 makubwa ya akiba Tanzania, mikoa iliyopo, ukubwa wake na fursa za kitalii zinazoweza kupatikana katika rasirimali hizo.

Uchambuzi wa takwimu muhimu za mwaka 2018 za Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Tanzania in figures 2018) uliofanywa na Nukta unabainisha kuwa mapori hayo ya akiba kwa ujumla wake yana ukubwa wa kilomita za mraba 96,146 ambazo ni sawa na  takribani mikoa sita ya Dar es Salaam, Songwe, Mara, Njombe, Geita na Rukwa. 

Ifuatayo ni orodha ya mapori 10  ya akiba makubwa zaidi  Tanzania: –

1.Pori la Akiba la Selous (Selous Game reserve)

Selous ndiyo pori kubwa zaidi kuliko yote nchini likiwa na ukubwa wa kilomita za mraba zipatazo 50,000 lipatikana katika mikoa minne ya Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara na Ruvuma. Pia, Selous ambalo linachukua nusu ya eneo lote la mapori ya akiba Tanzania, linashika  nafasi ya pili kwa ukubwa  barani Afika.

Pori hilo, lilianzishwa mwaka 1896 na kuchapishwa kwenye gazeti la serikali la kijerumani mwaka 1905 (gazetted by colonial Germany government in 1905).

Ndani ya Selous kuna makundi makubwa ya tembo  sambamba na aina 430 za ndege. Wanyama wengine wanaopatikana katika pori hilo ni chui, kifaru viboko simba ,mbwa ,mwitu , fisi na mamba.

Ili mtalii aweze kufika, anaweza kutumia usafiri wa ndege, barabara au kwa treni ya Tazara. Usafiri wa barabara kutoka  Dar es Salaam hadi Matambwe kupitia Morogoro ni kilomita 275 wakati kutoka Dar es Salaam mpaka Mtemere kisha Mloka ni kilomita 185.

Ndani ya Selous kuna makundi makubwa ya tembo  sambamba na aina 430 za ndege. Picha|Mtandao. 

Ukitaka kutumia treni ya Tazara pia unaweza kufika huko hadi Matambwe station. Utalii unao wezakufanyika huko ni pamoja na uwindaji,upigaji picha,utalii wakutembea na wamajini katika mto Rufiji.

Hata hivyo, siku si nyingi sehemu ya pori hilo itamegwa na kuanzisha hifadhi mpya ya Taifa ya Mwalimu Nyerere baada ya Rais John Magufuli kuagiza hatua hiyo mwishoni Julai mwaka huu.

2. Rungwa

Pori la akiba la Rungwa ni la pili kwa ukubwa Tanzania likiwa linaingia takribani mara sita ya pori la akiba la Selous. Pori hilo, lililoanzishwa mwaka 1951 kabla ya Uhuru, lina kilomita za mraba 9,000 linapatikana katika mikoa ya Tabora, Singida na Mbeya.

Baadhi ya wanyama wanaopatikana katika pori hili la akiba ni simba, fisi , swala tembo na nyati. Mtalii akiwa katika pori hili la akiba anaweza pia kuwinda.

Mtalii anaweza kufika kwenye pori hilo la akiba kwa kutumia ndege ndogo na kutua katika kiwanja kidogo kilichopo hapo au kwa njia ya gari kutokea Manyoni mpaka Rungwa. Iwapo anatokea Mbeya, mtalii huyo atatakiwa kupitia Chunya hadi Rungwa.

Mbali na utalii wa wanyama, pia kuna fursa za uwekezaji kama utalii wa uwindaji na hoteli.

3.Kigosi

Kigosiu ni pori la akiba lenye ukubwa wa kilomita za mraba zipatazo  7,000 na kufanya kuwa pori la tatu la akiba kwa ukubwa Tanzania. 

Likipatikana katika mikoa ya Tabora na Shinyanga, Kigosi lilianzishwa mwaka 1981 na kama yaliyo mapori mengine linajumuisha wanyama wakali na ndege mbalimbali wakiwemo Simba, mamba na bata.

Mbali na kutazama wanyama, ukiwa katika pori hilo unaweza kuwinda na kuvua samaki. 

Ili kuweza kupata huduma hiyo, Kigosi panafikika kwa ndege, boti na barabara vile vile mtu anaweza kuwekeza kwenye upigaji picha na utalii wa kutazama ndege (bird watching).


Zinazohusiana:


4.Moyowosi

Ni pori la akiba lilionzishwa mwaka 1983 na lina ukubwa wa kilomita za mraba zipatazo 6000. Pori la Monyowosi lipo magharibi mwa Tanzania mkoani Kigoma karibia na mwambao wa Ziwa Tanganyika.

Eneo hilo linaweza kufikika kwa barabara, ndege ndogo na hata kwa treni kuanzia Dar es Salaam hadi Kigoma. Baadhi ya wanyama waliopo ni simba, bata na viboko.

5.Ugalla

Ugalla ni pori la akiba lililopo mkoani Tabora lenye ukubwa  wa kilometa za mraba zipatazo 5,000 na lilianzishwa mwaka 1965. Wanyama ambao unaweza kuwaona ni chui, simba, nguruwe pori, mbwa mwitu pundamilia, swala na fisi.

Ukiwa ndani ya pori hilo pia unaweza kufanya utalii wa kuwinda wanyama, wa kutembea na uvuvi wa kitalii kwa kutumia ndoana (sport fishing).

Ili kufika huku, itakubidi kusafiri zaidi ya kilomita 100 kutoka Tabora mjini wakati wa kiangazi na ndege ndogo zinaweza kutia katika viwanja vidogo vya  Muhuba and Siri.

Ukiwa ndani ya pori hilo pia unaweza kufanya utalii wa kuwinda wanyama, wa kutembea na uvuvi wa kitalii kwa kutumia ndoana (sport fishing). Picha|Mtandao. 

6.Uwanda

Pori la akiba la Uwanda linachukua takribani asilimia 80 ya eneo la Ziwa Rukwa lilipo kaskazini Mashariki mwa Tanzania .

Pori hilo lilianzishwa mwaka 1974 na lina kilomita za mraba sawa  na pori la akiba la ugalla zipatazo  kil#omoita za mraba 5,000. Uwanda nalo lipo vizuri kwa wanyama pori likiwa ni hifadhi ya tembo na nyati.

Panafikika kwa ndege  gari lenye  wa kupita mahali popote pale (four  wheel drive)

7.Kizigo

Pori la akiba la Kizigo lina ukubwa wa kilimita za mraba zipatazo 4,000s ilianzishwa mwaka 1951 na linapatikana katika mkoa wa Singida. Mtalii akiwa katika pori hilo ataweza kuona wanyama kama tembo, swala, pundamilia, simba na fisi.

Vile vile mtalii ataweza kufanya uwindaji. Iwapo unataka kufanya utalii huko unaweza kutumia usafiri wa ndege au barabara.

Kwa wale wanaosaka fursa za kuwekeza, eneo hili wanaweza kuwekeza katika utalii wa uwindaji na hoteli.

8.Rukwa

Likiwa Kusini Magharibi mwa Tanzania, Rukwa ni pori la akiba linalopatikana katika mikoa miwili ya Rukwa na Katavi. Pori hilo lina ukubwa wa kilimita za mraba  zipatazo 4,000 na linajulikana zaidi kwa kuwa na idadi kubwa ya mamba wanaopatikana katika mwambao wa Mto Rukwa.

Pori hilo lina wananyama kama twiga, simba, mbwa mwitu, swala na viboko.

Kama wewe ni mtali usitie shaka unaweza kufika mpaka kwenye eneo hilo kwa kutumia ndege ndogo hadi katika uwanja ulipo katika hifadhi ya Taifa ya Katavi.

Vile vile kwa kutumia barabara unaweza kufika hadi kwenye pori la akiba la Rukwa mathalani ukitokea  Dar es Salaam kupitia Tunduma ni kilomita 1,421.

Pori hilo lina wananyama kama twiga, simba, mbwa mwitu, swala na viboko. Picha|Mtandao. 

9.Lukwati

Ni pori la akiba la tisa kwa ukubwa nchini Tanzania likiwa na kilomita  za mraba zipatazo 3,146 likiwa linapatikana katika maeneo ya Katavi/Rukwa Tanzania. Pori linaingia mara  15 kwa Selous linaloongoza kwa ukubwa nchini. 

10.Ikorongo

Pori la akiba la Ikorongo ni pori la 10 kwa ukubwa Tanzania likiwa na na ukubwa wa kilomita za mraba 3000 , linaingia takribani mara 16 ya pori la Selou.Pori hili lilianzishwa mwaka 1994 na linapatikana wilaya za Bunda and Serengeti mkoani Mara.

Ikorongo ni pori la akiba lenye aina mbalimbali za wanyama kama tembo, fisi, pundamilia , mbwa , mwitu na  kifaru.

Mtalii naweza kufika kwenye pori la akiba la Ikorongo kwa njia ya barabara kutokea Arusha kupitia Ngorongoro kisha Serengeti. Kwa watalii wanatokea Mwanza wanaweza pitia Bunda kisha Mugumu mpaka kwenye pori hilo la akiba.

Pia mtu anaweza kuwekeza kwenye pori hilo la akiba hususani kwenye uwindaji na upigaji picha za utalii.