October 6, 2024

Mambo ya kuzingatia tovuti yako isomwe na watu wengi

Mambo hayo ni pamoja na kuweka taarifa sahihi zilizosanifiwa kwa lugha nyepesi inayoeleweka haraka.

  • Weka taarifa sahihi zilizosanifiwa kwa lugha nyepesi inayoeleweka haraka. 
  • Unaweza kutumia viunganishi na mitandao ya kijamii ili kuvuta watu wengi wakutembelee. 

Dar es Salaam. Ni ndoto za wamiliki wa tovuti mbalimbali kupata wasomaji wengi na kwa muda mrefu ili kutimiza malengo ya kuzianzisha, iwe kwa ajili ya bidhaa au huduma na taasisi husika.

Kuna mambo mbalimbali ya kuzingatia katika kufanya tovuti yako iwe na wasomaji wengi na kuwafanya waifuatilie kwa muda mrefu.  Mtandao wa CMS Wire wamekuletea mambo sita yatakayokusaidia kama mmiliki wa tovuti kupata watu wanaotembelea tovuti yake kwa muda mrefu.

Kitu cha kwanza ni kuwa makini na taarifa unazotaka ziwafikie watu wako. Kwa taarifa unazoweka katika tovuti yako ndizo zinazosaida katika kupata watu makini watakaokua wanatembelea tovuti yako.

Namna unavyomshawishi msomaji kwa picha ni kitu kingine kwa sababu picha ni moja ya vitu vinavyomsogeza au kumvutia msomaji. Unashauriwa kutumia picha, video katika taarifa zako ili kufikisha ujumbe kwa njia rahisi zaidi. 

Matumizi ya lugha nyepesi na fupi pia ni muhimu. Msomaji anataka anaposoma kwa mara ya kwanza apate maana ya kitu kuliko kutumia muda mwingi katika kusoma kitu ambacho kitamchukua muda mrefu kuelewa.


 Soma zaidi: Una mpango wa kuipeleka biashara mtandaoni? Zingatia haya


Mpangilio wa mwelekeo wa maandishi yako lazima yawe yameanza upande wa kushoto kwenda kulia kwa sababu ndio utaratibu uliozoeleka ili asome bila ya kupata tabu yoyote kwa namna ambavyo maandishi yanakwenda.

Kuonyesha maneno yaliyo na msisitizo kwa kuyakoleza na kuunganisha na kiunganishi husika (Hyperlink) pia ni jambo lingine la kuzingatia kwa sababu mtu atapata maana na kuvutiwa kusoma zaidi ili apate taarifa zitakazomfaidisha. 

Mtiririko wa mawazo yako pia ni muhimu upangwe vizuri. Watu wengine wanaweza wakavutiwa na namna ulivyoanza kupanga mawazo yako ya uandishi wako kuwapa hamu ya kusoma zaidi maandiko yako. 

Matumizi ya lugha nyepesi na fupi pia ni muhimu. Msomaji anataka anaposoma kwa mara ya kwanza apate maana ya kitu kuliko kutumia muda mwingi katika kusoma kitu ambacho kitamchukua muda mrefu kuelewa. Picha|Mtandao. 

Naye mtaalam wa programu za kompyuta, Khadija Mahanga  amesema mitandao ya kijamii na matumizi ya viunganishi (links) pia yanaweza kusaidia kuwavutia watu wengi kutembelea tovuti yako. 

“Kuhakikisha viunganishi vimepangiliwa vizuri pamoja na maneno kueleweka na matumizi mazuri ya mitandao ya kijamii ni vitu muhimu sana katika kufanya tovuti yako ipate watu wanaosoma au wanaotembelea,” amesema Mahanga.

Huenda dondoo hizi zikakusaidia kupata watu wengi ambao wataongeza thamani ya huduma na bidhaa kwa kukuongezea wigo wa soko na kipato.