July 8, 2024

Maumivu yaja kwa wacheza michezo ya kubahatisha

Serikali imebuni mfumo wa kudhibiti michezo hiyo ili kujipatia zaidi mapato ya kodi.

  • Serikali imebuni mfumo wa kudhibiti michezo hiyo ili kujipatia zaidi mapato ya kodi.
  • Pia utadhibiti udangajifu unaofanywa na waendeshaji wa michezo hiyo. 

Dar es Salaam. Serikali imebuni na kutengeneza mfumo wa kudhibiti michezo ya kubahatisha maarufu kama ‘betting’ ikiwa ni hatua ya kuongeza mapato baada ya kuonekana una muitikio mkubwa wa watu hasa vijana. 

Hatua hiyo inakuja ikiwa imepita miezi sita tangu Makamu Mwenyekiti wa dhehebu la Mabohora, Zainuddin Adamjee kulalamika mbele ya Rais John Magufuli, Ikulu jijini Dar es Salaam kuwa nguvukazi ya Taifa inapotea kwa sababu vijana wengi hawafanyi kazi na wanatumia muda mwingi kucheza michezo hiyo kwenye mitandao ya kijamii. 

Wakati akiwasilisha mapendekezo ya bajeti ya Serikali kwa mwaka 2019/2020, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amesema kuwa kutokana wimbi la vijana wengi kujihusisha na michezo ya kubahatisha na kusahau majukumu ya ujenzi wa Taifa,  Serikali imependekeza kutengeneza mfumo maalum wa kudhibiti uendeshaji wa michezo hiyo. 

“Serikali ikishirikiana na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha imebuni na kutengeneza mfumo maalum ambao utatumika kudhibiti uchezaji  wa michezo hii (Responsible Gaming),’ amesema Dk Mpango.

Waziri huyo amesema Serikali imependekeza mfumo huu kutumika ili kudhibiti udanganyifu ambao unafanywa na waendeshaji wa michezo ya kubahatisha na kuikosesha Serikali mapato.