July 8, 2024

Namna ya kuepuka madhara wakati ukitumia vifaa vya umeme nyumbani

Zingatia kusoma maelekezo vizuri yaliyowekwa kwenye vifaa hivyo kabla ya kutumia.

  • Epuka kushika vifaa vya umeme ukiwa na maji.
  • Zingatia kusoma maelekezo vizuri yaliyowekwa kwenye vifaa hivyo kabla ya kutumia.

Dar es Salaam. Ni wazi kwamba matumizi ya vifaa vya umeme kama friji, pasi na majiko ni vitu cha kawaida  tukiwa nyumbani katika kufanikisha shughuli mbalimbali kwa urahisi.

Lakini uangalifu mkubwa unahitajika katika matumizi ya vifaa hivyo ili kuepukana na hatari za kupata majanga yanayoweza kusababishwa na matumizi yasiyo sahihi ya vifaa hivyo kama kupata majeraha, ulemavu au kupoteza maisha. Zingatia haya ukiwa unatumia vifaa hivyo nyumbani;

Epuka kutumia vifaa vya umeme ukiwa umetoka kushika maji. Henda ukawa mmoja ya watu wanaopenda kutumia vifaa vya umeme ukiwa umetoka kushika maji. Tabia hii inaweza kukumaliza endapo utashindwa kuiacha

Moja ya vitu visivyoendana na umeme ni maji. Katika matumizi ya vifaa hivi, unapotoka kushika maji ni vyema ukahakikisha umejikausha mikono sawa sawa kabla ya kushika kifaa chochote cha umeme. Kwa kufanya hivyo, unaepukana na balaa la kurushwa au hatari nyingine yoyote kubwa inayosababishwa na umeme.

Hakikisha vishikio vya pasi au mlango wa friji vina plastiki au kishikio chochote na siyo chuma pekee. Mshikio wa kifaa chochote kinachotumia umeme kama pasi, mlango wa jokofu au hata  jiko la kupashia chakula (oven) inapaswa kuwa imezungushiwa plastiki ili kuepusha balaa lililopo kwa chuma kubaki bila mshikio na kusababisha hatari kwa urahisi kuliko ikiwa imezungushiwa na plastiki.


Zinazohusiana:


Tumia viatu ukiwa unatumia kifaa chochote cha umeme. Ukiwa unatumia kifaa chochote cha umeme, inashauriwa kuwa na ndala ili kukata uhusiano kati ya mwili wa binadamu na umeme.

Fundi umeme kutoka Kinondoni jijini Dar es Salaam, Denis Mbogo amesema pale mtu anapotumia kifaa chchote cha umeme endapo kuna hitilafu yoyote, mwili wa binadamu unaweza kuwa kiunganishi cha kusafirishia umeme ambayo ni hatari inaweza kusababisha kifo.

“Ukiwa unatumia umeme ndani, ni  bora utumie ndala kama silaha. Bila ndala halafu ikatokea shida mwili wako unakuwa waya badala ya kifaa, kifuatacho hapo ni kifo kwa sababu umeme utapita pia mwilini mwako,”amesema Mbogo.

Hata hivyo, sambamba na hayo, ukisoma vizuri maelekezo ya matumizi ya vifaa hivi baada ya kununua ni rahisi kujua vitu vya kuzingatia ili kuzidi kujikinga na hatari za kupata madhara ukiwa unatumia vifaa hivyo nyumbani.