October 6, 2024

Shule ya kwanza ya mafunzo ya ndege zinazoruka bila rubani yafunguliwa Malawi

Shule ya kwanza Afrika ya mafunzo ya ndege zinazoruka bila rubani (Drone) na takwimu imefunguliwa Lilongwe, nchini Malawi ili kuchagiza programu za utoaji huduma za misaada barani Afrika hasa kwa watoto na vijana.

Kufikia mwaka 2022,  ADDA itaendesha programu ya shahada ya uzamili kuhusu teknolojia ya ndege zinazoruka bila rubani ya miaka miwili bila malipo kwa ushirikiano na Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Malawi. Picha|UNICEF/Brown.


  • Inakusudia kutoa mafunzo wa wanafunzi takriban 150 kujenga na kurusha ndege zinazoruka bila rubani kufikia mwaka 2021.
  • Ndege hizo zitatumika kurahisisha shughuli za utoaji was misaada ya kibinadamu hasa kwa watoto na vijana.

Shule ya kwanza Afrika ya mafunzo ya ndege zinazoruka bila rubani (Drone) na takwimu imefunguliwa Lilongwe, nchini Malawi ili kuchagiza programu za utoaji huduma za misaada barani Afrika hasa kwa watoto na vijana.

Kwa mujibu taarifa iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF), shule hiyo (first African Drone and Data Academy (ADDA)) imefunguliwa Januati 13 mwaka huu.

Hatua hiyo ni katika juhudi za kuimarisha matumizi ya ndege zinazoruka bila rubani katika programu na huduma ambazo zitaboredha maisha ya watoto na vijana.

Mkurugenzi Mkuu wa UNICEF, Henrietta Fore amesema programu za misaada ya kibinadamu na maendeleo barani Afrika zinaweza kunufaika kwa kiasi kikubwa kutokana na matumizi ya teknolojia ya ndege zinazoruka bila rubani.

 â€œshule ya Afrika ya ndege zinazoruka bila rubani na takwimu itakuwa na mchango mkubwa katika kuwajengea vijana stadi wanazozihitaji katika kutumia teknolojia hiyo kwa ajili ya watoto wao na jamii,” amenukuliwa Fore katika taarifa ya Umoja wa Mataifa (UN) wakati wa uzinduzi wa shule hiyo.

Katika kuendeleza kazi ya misaada ya kibinadamu Afrika shule hiyo iliyozinduliwa Malawi itaimarisha ustadi wa matumizi ya ndege hizo kwa ajili ya shughuli za kibinadamu, maendeleo na biashara barani Afrika kupitia mafunzo ya wiki 12 ambapo inakadiria kutoa mafunzo wa wanafunzi takriban 150 kujenga na kurusha ndege zinazoruka bila rubani kufikia mwaka 2021.


Soma zaidi:


Ufadhili kutoka kwa wadau wa UNICEF utatoa fursa kwa wanafunzi 26 kutoka Afrika kusoma bila malipo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kitengo cha Shirika la masuala ya anga la Malawi, James Chakwera amesema nchi hiyo inaamini kuwa kukumbatia teknolojia za kisasa kwa mfano ndege zinazoruka bila rubani na tathmini bora ya takwimu na usimamizi kutatusaidia kuhudumia watoto wa Afrika kutimiza malengo yao.

“Tunafuraha kuungana na UNICEF katika ushirkiano huu mzuri,” amesema Chakwera katika taarifa hiyo.

Mtaala wa kozi zitakazofundishwa katika shule hiyo umetengenezwa kwa ushirikiano na taasisi ya mafunzo ya Virginia na Chuo Kikuu cha Virginia cha Marekani kufuatia warsha zao za mafunzo nchini Malawi tangu 2017 ambapo mafunzo yatajumuisha mafunzo darasani na vitendo ikiwemo ya kukarabati na kurusha ndege hizo.

Kufikia mwaka 2022,  ADDA itaendesha programu ya shahada ya uzamili kuhusu teknolojia ya ndege zinazoruka bila rubani ya miaka miwili bila malipo kwa ushirikiano na Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Malawi.