October 6, 2024

Kutana na app inayokusogezea huduma za afya nyumbani kwako

Mtu anawezeshwa kuingia kuingia kwenye programu hiyo na kuangalia vituo vya afya vilivyopo karibu au kupata mawasiliano ya daktari ili kumpa ushauri wa hatua za awali za kuchukua kudhibiti changamoto ya kiafya aliyopata kwa wakati husika.

Ili mtu atumie anapaswa kuwa na simu janja iliyounganishwa na intaneti kwa sababu huduma zake ni bure, anachotakiwa ni kuipakua tu kutoka kwenye duka la mtandaoni la Play store. Picha|Afya Time.


  • Inamwezesha mgonjwa kupata ushauri wa kiafya kutoka kwa daktari kupitia simu ya mkononi.
  • Ni programu tumishi ya Afya Time inayotumika katika simu za Android.
  • Inalenga kufikia watumiaji wa mfumo wa iOS siku zijazo.

Dar es Salaam. Unaweza kuwa mmoja wa watu  wanaopata changamoto ya kutafuta huduma za afya pindi unapojisikia kuumwa ukiwa mbali na kituo cha afya au maduka ya madawa.

Kampuni ya Bluefin Solution Limited wamebuni programu tumishi ya simu za Android ya Afya Time  inayomwezesha mgonjwa kuwasiliana na daktari kwa ajili ya ushauri pale inapohitajika.

Mgonjwa anawezeshwa kuingia kuingia kwenye programu hiyo na kuangalia vituo vya afya vilivyopo karibu au kupata mawasiliano ya daktari ili kumpa ushauri wa hatua za awali za kuchukua kudhibiti changamoto ya kiafya aliyopata kwa wakati husika.

Pia inampa mtu urahisi wa kuchukua hatua haraka pale anapojiskia vibaya kwa kupata ushauri kutoka kwa madaktari waliojiunga na programu tumishi hiyo, nini anatakiwa kufanya au ushauri wa kumwelekeza kwenda kwenye kituo cha afya kilichopo karibu nae.

Ili mtu atumie anapaswa kuwa na simu janja iliyounganishwa na intaneti kwa sababu huduma zake ni bure, anachotakiwa ni kuipakua tu kutoka kwenye duka la mtandaoni la Play store.


Soma zaidi:  


Mratibu wa programu hiyo, Brian Mallya ameiambia www.nukta.co.tz kuwa programu hiyo inatatua changamoto ya mgonjwa kukaa na tatizo kwa muda mrefu bila kupata ushauri wa daktari wa nini anatakiwa kufanya katika hatua za awali za tatizo.

“Kwa application (programu tumishi) hii mgonjwa ana uwezo wa kuwa na kuwasiliana na daktari muda wowote kwa kupata ushauri wa kitaalamu anaoweza kuchukua mgonjwa,kituo cha afya cha karibu cha kutembelea au hatua muhimu za kuchukua mwanzoni,” amesema Brian.

Kwa sasa, programu hiyo imeanza kufanya kazi na hospitali zisizopungua nne na tayari imewafikia watu zaidi ya 600 katika maeneo mbalimbali Tanzania hasa mkoa wa Dar es Salaam, ikilenga kujitanua katika maeneo mengine.

Kwa sasa, programu hyo haijawafikia watumiaji wa simu zinazotumia mfumo wa iOS unaotumiwa na simu za Iphone lakini wako katika mchakato wa kuwafikia watumiaji wote wa simu za mkononi.

Programu hiyo siyo ya kwanza Tanzania kutoa huduma za afya kwa njia ya mtandao, nyingine ni pamoja na  Life Plus na Afya Pap.