July 8, 2024

Facebook yaingia 10 bora ya programu zinazopakuliwa zaidi mtandaoni

Programu nyingine zilizoingia kwenye orodha hiyo ni pamoja na Messenger, Instagram, Whatsapp,Twitter, Snapchat, Tiktok na Skype.

  • Programu nyingine zilizoingia kwenye orodha hiyo ni pamoja na Messenger, Instagram, Whatsapp,Twitter, Snapchat, Tiktok na Skype.
  • Programu hizo za simu zimekuwa kiungo muhimu cha mawasiliano duniani.

Dar es Salaam. Ndoto ya kufikia malengo katika biashara ni matamanio ya kampuni yoyote duniani hasa pale yanapotimia katika muda muafaka. 

Huenda mtandao wa Facebook ukahitimisha mwaka 2019 kwa kishindo, baada ya sehemu kubwa kukamilisha mipango yake iliyojiwekea miaka 10 iliyopita. 

Mtandao huo ulioanzishwa na raia wa Marekani, Mark Zuckerberg umefanikiwa kumiliki programu tumishi za simu nne kati ya mwaka 2010 na 2019 ambazo zimekuwa kiungo muhimu cha mawasiliano duniani. 

Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na kampuni ya uchambuzi wa programu tumishi ya  App Annie imeonyesha namna kampuni hiyo ilivyoweza kufikia moja kati ya malengo yake kwa kipindi cha miaka kumi, kwa kuwakutanisha watu dunia nzima kupitia mitandao ya kijamii.

Programu hizo ni Facebook ambayo imezaa Messanger, WhatsApp na Instagram zinazotumika kuunganisha ndugu, jamaa na marafiki katika maeneo mbalimbali duniani.

Pia, zimetangazwa kama programu tumishi nne zinazoongoza kati ya 10 kwa kupakuliwa na watumiaji wengi katika kipindi cha miaka 10 mfululizo.


Zinazohusiana:


Mafanikio hayo ni hatua kubwa kwa mtandao wa Facebook kwani kumekuwa na changamoto nyingi na maboresho ya mtandao huo yaliyosaidia mtandao huo kufika ile hatua iliyokusudiwa. 

Programu tumishi nyingine ambazo zimeingia 10 bora ya kupakuliwa zaidi duniani ni pamoja na Snapchat inayomilikiwa na kampuni ya Snap ya Marekani, Skype iliyopo chini ya Microsoft na Tiktok chini ya ByteDance. 

Nyingine ni Uc Browser inayomilikiwa na kampuni ya Alibaba, YouTube chini ya Google na Twitter.