October 6, 2024

Yakuzingatia wakati wa unanunua vifaa vya muziki

Ndiyo, geto la mshikaji bila mfumo wa sauti huenda likaonekana kama halijakamilika hivi kwani mbali na kusikiliza muziki, huenda mfumo wa sauti ukatumika kwa shughuli zingine zikiwemo kupunguza kelele za majirani zako.

  • Ubora wa sauti na uwezo wako wa fedha ni muhimu kabla ya kuingia dukani.
  • Mahitaji na mazingira unakoenda kutumia vifaa hivyo. 
  • Fanya utafiti kwanza wa “brand” unayoenda kununua na ubora wake. 

Dar es Salaam. Hakuna asiyependa mdundo na mfumo mzuri wa sauti (Sound System) unaotoka kwenye redio yenye spika za kueleweka.

Ndiyo, geto la mshikaji bila mfumo wa sauti huenda likaonekana kama halijakamilika hivi kwani mbali na kusikiliza muziki, huenda mfumo wa sauti ukatumika kwa shughuli zingine zikiwemo kupunguza kelele za majirani zako.

Ili kuwa katika mstari ulionyooka katika kununua vifaa hivyo vilivyo bora, unahitaji kuzingatia baadhi ya mambo ili kuepuka hasara na kupata mfumo wa sauti utakaopendeza masikio yako na usio kuwa kero kwa watu wanaokuzunguka. 

Ya kuzingatia kabla ya kununua ni yapi?

Ukubwa wa pochi yako

Ni kitu cha kwanza kabisa kufikiria kwani huwezi kununua kitu ambacho pesa yake hauna. Kuna mifumo mingi ya sauti na orodha yake hauwezi kuimaliza. Hivyo ukubwa wa mfuko wako ndiyo utakaokuwezesha kwenda dukani kifua mbele huku ukitamka “brand” ya mfumo unaohitaji.

Kwa mujibu wa huduma kwa mteja kutoka kampuni ya vifaa vya kielektroniki ya Samsung Tanzania, pochi yako ndiyo itakayokuwezesha kupata mfumo wa sauti unaoendana na mahitaji yako.

Mazingira na matumizi

Samsung imeiambia Nukta (www.nukta.co.tz) kuwa mifumo ya sauti ipo kutimiza mahitaji na matumizi ya kila aina.

“Kuna mifumo ya sauti inayofaa sebuleni na mifumo ya sauti inayofaa chumbani. Mara nyingi ni ukubwa wa eneo lako ndiyoo utakaoamua mfumo upi unakufaa,” imeeleza Samsung.

Mbali na hilo, matakwa ya mtumiaji pia huzingatiwa kwani wapo wanaopenda muziki wa juu na wale wanaopenda muziki wa wastani.

Kuna mifumo ya sauti iinayotumia waya na ile isiyotumia waya. kazi ni kwako kuchagua. Picha| Giphy.

“Brand” na sifa za wadau

Tovuti ya worldwidestereo imeorodhesha mifumo ya sauti bora zaidi kwa mwaka 2020 huku nafasi ya kwanza ikishikiliwa na Sonos 5.1 ambayo inagharimu takriban Sh3 milioni. Huenda bei ya mfumo huo wa sauti ikawa imekuzwa na teknolojia ya kisaidia sauti (voice assistant) ambacho kinakupa uwezo wa kuiendesha kwa kutumia sauti yako.

Ndiyo ni muziki tu! Kwa brand zingine zenye sifa zikiwemo  Bose Soundbar 700 (Sh4.13 milioni) na SVS Prime Satellite 5.1 (Sh2.29 milioni) inafaa kwa watu wenye nyumba ndogo.

Mbali na tafiti hii, unaweza kuwasiliana na washikaji wakakupatia mawazo juu ya mifumo waliyonayo kwenye nyumba zao ili upate pa kuanzia.

Ubora wa sauti

Hiki ni kitu muhimu kuzingatia pia kwani hakuna asiyependa mdundo wa redio mbao anaposikiliza ngoma zake sebuleni na hata chumbani kwake. Hivyo kufanya uwepo umuhimu wa kununua mfumo wa sauti wenye kutoa sauti murua.

Kwa kufanya hivyo, hata majirani hawatalalama ukifungulia muziki zaidi bali watakugongea kuuliza ni mfumo gani unatumia.


Zinazohusiana


Viambatanishi vya mfumo huo

Mike Roosevelt ambaye ni mdau wa masuala ya kompyuta mwenye makazi yake Jijini Dar esSalaam amesema kwa yeye anazingatia kununua mfumo ambao unaendana na harakati zake.

“Kuna mifumo inatumia teknolojia ya deki na ambayo haina teknolojia hiyo. Kwa mimi ambaye ninapenda kuangalia filamu, deki au sehemu ya flashi ni muhimu kwangu hivyo nikienda kununua “mdundo” wangu lazima uwe na hivyo vitu,” amesema Roosevelt.

Ubora wa mfumo huo

Kwa kuwa ipo mifumo mingi sokoni, ni muhimu kuangalia ubora wa mifumo hiyo ili kuepukana na shuruba za kuhangaika na mafundi baada ya siku chache tu za manunuzi.

Sise Christopher ni kati ya wadau wa muziki wa jijini dar es Salaam amesema amewahi kununua spika ambayo haikudumu hata miezi miwili.

Christopher angeepuka usumbufu huo kama angekuwa makini kununua mfumo mzuri wa sauti. 

Baada ya kuyafahamu hayo, sasa unaweza kwenda dukani kifua mbele na kuchagua mfumo unaoumudu. Hata hivyo, ni vizuri kufanya utafiti  kabla ya kutimba dukani kwa ajili ya manunuzi.